SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI

Siku ya Mazingira Duniani huadhimishwa kila Juni 5. Siku ya leo ni miaka 50 tangu maadhimisho haya yalipoanza rasmi mwaka 1973. Sababu za kuadhimisha ni kukumbushana juu ya umuhimu wa mazingira kwa ustawi wa mtu mmoja mmoja, jamii na ikolojia. Tanzania, kama nchi huadhimisha siku hii. Maadhimisho haya ni muhimu kwa nchi na serikali. Kama nchi tunaungana na wenzetu ili kulinda nyumba yetu yaani Dunia. Hali kadhalika Serikali ina jukumu la kulinda ustawi wa watu. Kuadhimisha siku hii ni kutekeleza jukumu la ulinzi. Sisi kama wa-Tanzania ni wanufaika wa kudra za mazingira. Sisi ni wanufaika wa kimazingira kwani Tanzania tofauti na nchi nyingine ni tajiri wa ardhi yenye rutuba, vyanzo vingi vya maji, misitu, na wanyamapori.


Hali kadhalika Tanzania ni tajiri wa gesi asilia na mafuta. Rasilimali hizi zinaendelea kutunufaisha kama nchi. Kwa bahati mbaya zinakutana na changamoto nyingi pia. Utegemezi wetu umeongezeka. Kwingineko tunaiona jamii ikivuna kinyume na taratibu. Uhitaji wa mashamba, maji, madini nao umebabisha kuharibika kwa baadhi ya rasilimali hizi. Uharibifu huu unanyanyasa jamii ya sasa na kuweka changamoto kwa vizazi vinavyokuja. Timu ya Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) inasherehekea siku hii kwa kukumbusha jamii juu ya umuhimu wa mazingira. Kwa pamoja tunawajibu kulinda mazingira na rasilimali zake. Uharibifu wa mazingira ni vyanzo vya magonjwa, kupanda kwa bei ya maisha, na kukosekana na amani na usalama. 


LEAT na shughuli zake inaendelea kuangazia maeneo mbalimbali, yakiwemo: (a) mabadiliko ya tabianchi; (b) uchafuzi wa taka ngumu (ikiwemo plastiki); (c) kelele; na (d) ulinzi wa vyanzo vya maji.

MABADILIKO YA TABIANCHI

Tanzania ni mshirika muhimu kukabilina na mabadiliko ya tabianchi. Nafasi ya nchi kijiographia kunaipa Tanzania nafasi adhimu. Uwepo wa sehemu kubwa ya viumbe hai (hotspot) sita kati ya 25 ni fursa ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Katika kuungana na nchi nyingine Tanzania ni mdau wa IPCC, CBD, UNFCCC n.k.



  1. Tanzania inahitaji sheria mahususi ya Mabadiliko ya Tabianchi. Kwa hali ilivyo mabadiliko ya Tabianchi yanasimamiwa na Sheria ya mazingira namba 20, 2004. Ni kifungu cha 75 tu cha sheria kinasimamia mabadiliko ya Tabianchi. Tukumbuke hata kanuni mpya za kusimamia soko la hewa ukaa zimetungwa chini ya kifungu cha 75. Ni wakati sasa, Mabadiliko ya tabianchi yasimamiwe na sheria yake. Hii itamaanisha taasisi, mamlaka, sheria, kanuni na miongozo itatungwa kwa kufuata sheria mahususi ya mabadiliko ya tabianchi.

  2. Mchakato wa mapitio ya sheria ya mazingira uweke rasilimali nyingi kufikia wadau ili kuandaa sheria madhubuti na inayotekeleza itakayosimamia mazingira. Kudhibiti shughuli zinazozalisha mabadiliko ya Tabianchi iwe kipaumbele. Haya yaende sambamba na utaratibu wa kisheria wa kuwezesha jamii kuishi na mabadiliko ya tabianchi.


PLASTIKI

Ndoto za ukuaji kiuchumi, maendeleo ya viwanda na mahitaji ya kila siku ya binadamu yanaleta ugumu kusimamia plastiki. Pamoja na marufuku ya mifuko ya plastiki bado kwa nyakati tofauti mamlaka zimesikika zikikemea plastiki. Chupa za plastiki zitumikazo mara moja bado ni changamoto kubwa nchini. Ni vema:

  1. Malighafi za uzalishaji wa plastiki zikapigwa marufuku.

  2. Mamlaka zikapewa nguvu kutekeleza sheria zinazosimamia taka hasa kwenye mitaa na vijiji.

  3. Wazalisha plastiki wakakabiliwa.




UKUSANYAJI TAKA

Udhibiti wa taka umechukua mikondo tofauti. Wakati wa mamlaka za chini kuimarisha usimamizi wa sheria. Kaya lazima ziwe na miundombinu sahihi.  

  1. Kampuni za uzalishaji taka zikawezeshwa

  2. Ukusanyaji, na uchakataji wa taka ukaratibiwa vyema zaidi

  3. Maeneo mahususi ya uzalishaji taka yakafungamanishwa na urejelezaji




KELELE


Kelele zinaendelea kuwa changamoto kubwa nchini. Changamoto hii inaendelea pamoja na Sheria ya Mazingira Na. 20, 2004 inakataza kelele. Kifungu cha 140(1)d kinatangaza Tume ya Taifa ya Viwango vya Mazingira (National Environmental Standards Committee) chini ya Shirika la Viwanga Tanzania kuweka viwango vya sauti. Kifungu cha 141 cha Sheria ya Usimamizi wa Mazingira kinamtaka kila mtu kuheshimu viwango vilivyowekwa. Na kimahususi kabisa kifungu cha 147 kinazungumza juu ya sauti na mitetemo.


SWALI NI JE UNATAMBUAJE HII NI KELELE: TBS kama shirika la viwango limeweka kiwango cha sauti. Hivyo yoyote anayezidisha zaidi anakuwa ameleta kero ya kelele. Kuna applications nyingi mtandaoni zinazotambua viwango vya kalele (zinapatikana Play Store na App Store). Kanuni hizo hizo husimamia mitetemo. Na ndio maana kabla ya mgodi kupiga baruti hutangaza ili kupunguza mistake itokanayo na mitetemo (si mara zote hufanya hivi na waathirika wa mitetemo wapo maeneo mbalimbali ya nchi).


Halmashauri zimekuwa na sheria ndogo zinazosimamia mazingira. Baadhi ya sheria ndogo hizi hutoa makatazo na kuainisha adhabu kwa mpiga kelele/anayesababisha kelele.


Hali kadhalika sheria ndogo zinaainisha maafisa/afisa mwenye mamlaka na utoaji vibali kwa shughuli mbalimbali zikiwemo zenye kelele. Maelezo juu yanaangazia Ofisi ya Makamu wa Raisi, Baraza la Mazingira Tanzania, Shirika la Viwango na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (halmashauri, mitaa, vijiji) kama wadhibiti wa kelele.



CHA KUFANYA:

(a) Baraza la Mazingira Tanzania kuendelea kutumia kanuni kushughulikia suala la muda.


(b) Ofisi ya Makamu wa Raisi, Baraza la Mazingira Tanzania, Shirika la Viwango na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (halmashauri, mitaa, vijiji) kuelimisha Watanzania juu ya viwango vya sauti, ukomo wake, na namna ya kutambua viwango.


(c) Halmashauri zote zihamasishwe kutunga na kusimamia sheria ndogo za mazingira, msisitizo ukiwekwa juu ya muda na eneo. Mamlaka hizi zipewe rasilimali za kutosha ikiwemo watu, vifaa na fadha.


(d) Wananchi wakatae kelele


VYANZO VYA MAJI.

Tanzania ni tajiri wa rasilimali maji. Ni sehemu ya nchi katika eneo la maziwa makuu. Ina mabonde tisa ya maji yaliyotawanyika nchi nzima. Pamoja na utajiri wa maji, bado kuna changamoto mbalimbali. Nyakati za ukame, wananchi hulalamika kukosa huduma ya maji. Mamlaka za ugawaji maji mijini na vijijini ni sehemu ya malalamiko. TANESCO kama mtoa huduma wa umeme hulalamika kukosa maji kuzalisha nishati. Ingawa Mabadiliko ya Tabianchi yamekuwa kichaka, bado kuna changamoto lukuki. Mazingira jirani na vyanzo vya maji ni duni. Upotevu wa maji huleta huleta unmasking. Jamii na serikali zao wameshindwa kutunza vyanzo. Sheria nyingi husimamia vyanzo nazo zimeshindwa. 




CHA KUFANYA:

  1. Usimamizi madhubuti wa sheria ya mazingira ambayo hutaja vyanzo, hubainisha makosa, na kuweka adhabu kwa makosa mbalimbali.

  2. Vijiji vihamasishwe kutunga na kusimamia sheria ndogo zinazosimamia vyanzo vya maji. Sheria hizi zisiende kinyume na taratibu zilizowekwa na sheria ya usimamizi wa mazingira, sheria ya usimamizi wa rasilimali maji, na sheria nyingine zinazosimamia maji.

  3. Mamlaka hasa za vijijini zipewe uwezo wa kusimamia utekelezaji wa sheria. Jumuiya za Watumia maji (maarufu WUA), jumuiya za usimamizi wa mabomba (maarufu CBWSO) na wananchi kwa ujumla wadai usimamizi sahihi na uwajibikaji wa watoa huduma na wapokea huduma.

  4. Halmashauri zipewe uwezo madhubuti wa kutambua mapema na kushughulika na changamoto zote zinazoathiri usimamizi wa maji.

  5. Kuboresha Ulipiaji wa Huduma za Kiikolojia (Payment for Ecosystem Services - PES). Mfano, mashamba makubwa, kampuni n.k. zinazotumia maji kwa uzalishaji na zilipe jamii za uwanda wa juu (upstream) ambazo mara zote hulazimika kuachana na kutimiza ndoto zao na mahitaji yao ili jamii za chini zinufaike na maji.

  6. Wachafuzi wakubwa kama kampuni za uchimbaji madini washughulikiwe kwa ukubwa wao. Tafiti zinaonesha ongezeko la heavy metals kwenye vyanzo vya maji. Zebaki (mercuri) na cyanide zinaongezeka kutokana na uchakataji wa madini. Hii huhatarisha maisha ya watu na viumbe vingine.

0
0
0

Our   Partners